Zitto Kabwe: Matokeo mabovu ya kidato cha nne ‘kwanza waziri lazima awajibike na naibu wake’

Matokeo yaKidato cha Nne ya namna hii (zaidi ya nusu ya wahitimu kupata sifuri) na takribani asilimia 90 kufeli kwa kupata daraja la nne na daraja la sifuri ni mwaka tatu sasa mfululizo. Matokeo yakitoka tunasema weeee mpaka povu linatoka. Baada ya wiki tumeshasahau na hakuna hatua yeyote. Lazima Uwajibikaji utokee.

 

kwanza Waziri lazima awajibike na Naibu wake na Katibu Mkuu na Kamishna. Najua kuwa haina uhusiano wa moja kwa moja maana matatizo ya elimu ni makubwa sana nchini. Lakini ni lazima kitu fulani kitokee ili kufanya mabadiliko. Uwajibikaji ni njia mojawapo inayoleta nidhamu na 'urgency' katika utendaji kazi.

 

Tumwambie Rais aichukue Wizara ya Elimu, yaani Waziri wa Elimu awe yeye (kuwe na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Elimu). Tumwambie matokeo yakibaki hivi mwakani na yeye atatoka. Najua wa mwakani ndio wapo kidato cha nne sasa na wana msingi mbaya tayari lakini sio jukumu letu kujipa majibu bali ni jukumu letu kuiambia Serikali hapana. Tuwape Masharti. Vinginevyo haya yatakwisha na mwakani itakuja nk.

 

Hawa watoto wanakwenda wapi? Mwaka jana tulisema mpango wa kujenga vyuo vya ufundi kila Halmashauri ya Wilaya uanze mara moja. Katika Bajeti Kivuli mwaka 2011 tulipiga hesabu kwamba tunahitaji tshs 720 bilioni katika kipindi cha miaka 5 ijayo kujenga vyuo vya ufundi vya VETA kila Wilaya. Tukawaambia badala ya kukopa kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii kulipana posho ni vema tukope kuwekeza kwenye elimu maana Elimu ni Hifadhi ya Jamii. Elimu yetu ya sasa inazalisha matabaka kwneye jamii na ni hatari sana kwa uhai wa Taifa.

 

Tunaweza kujidai kujenga madaraja na miji mipya. Tunaweza kujidai kujenga mabomba ya gesi na kusambaza umeme kila kijiji mpaka kwenye vyoo. Kama hakuna Elimu haya yote ni bure kabisa. Hata kukosa uvumilivu wa kiimani sasa hali itakuwa mbaya zaidi unapokuwa na Taifa la mambumbumbu. Waziri Kawambwa na wenzake watoke. Watoke SASA